WIZI kwenye chumba cha Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Adam Kighoma Malima (pichani) mwishoni mwa wiki iliyopita katika Hoteli ya Nashera mkoani Morogoro, umedaiwa kufanywa na mwanamke anayejiuza, maarufu kama changudoa.
Vyanzo vyetu mbalimbali mjini Morogoro vimedai kuwa mwanamke huyo siku hiyo ya tukio alionekana maeneo ya hoteli hiyo ambapo inadaiwa aliweza kuagiza soda na kunywa kisha kuondoka hotelini hapo na baada ya muda mfupi alirejea.
Habari zinasema, mwanamke huyo haikujulikana aliondokaje katika hoteli hiyo, hivyo watu kumlenga yeye kuwa ndiye mwizi baada ya habari za naibu waziri kuibiwa fedha na mali mbalimbali zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 23 kuzagaa.
Mpasha habari wetu mmoja amedai kuwa mwanamke huyo ambaye amekuwa akihusishwa na wizi pamoja na utapeli mbalimbali mkoani hapa, amekuwa akionekana katika baadhi ya hoteli kubwa.

